Monday, June 4, 2012

ZANZIBAR: Wa-Unguja na Wa-Pemba Waanza Kugawanyika!

Kiongozi Mmojawapo wa Viongozi wa Umasho Zanzibar!


ILE dhambi ya ubaguzi ambayo Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere alionya kwamba huiwezi kuachwa sawa na kula nyama ya mtu, imeanza kujidhihirisha visiwani Zanzibar, baada ya kusambazwa vipeperushi vinavyotaka wananchi wenye asili ya Kisiwa cha Pemba kuondoka Unguja.

Ikiwa ni zaidi ya miaka 17 tangu Mwalimu kutoa onyo hilo, dhambi hiyo ya ubaguzi imeanza kuwatafuna Wazanzibari katika kipindi ambacho Jumuiya ya Uamsho Mihadhara ya Kiislamu (Jumiki), inazidi kuhamasisha Wazanzibari kuukataa Muungano.

Waakati kundi hilo la Jumiki likitaka Zanzibar iwe dola huru, limeibuka jingine linalojitambulisha kama ‘Watu wa Unguja’ likisambaza vipeperushi vinavyolishutumu kundi hilo la Uamsho, kwamba wahusika wake ni wananchi wanaotoka Pemba, wakitaka kuvuruga amani ya Unguja.

Huku wakihusisha baadhi ya viongozi waandamizi wa Serikali ya Mapinduzi  (SMZ), katika vipeperushi.Hivyo wamemwomba Rais Jakaya Kikwete ashauriane na Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein wawaruhusu wapewe kisiwa chao cha Pemba.

“Watu wa Unguja tunatoa ujumbe mahususi kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Jakaya Kikwete…. Tumechoka kuishi na Wapemba katika kisiwa chetu cha Unguja, kwani ni watu wasio na fadhila ya aina yoyote ile,” inasomeka sehemu ya kipeperushi kimoja na kuongeza:,
“Hivyo, tunakuomba ufanye mazungumzo na Rais wa Zanzibar ili Wapemba wapewe kisiwa chao cha Pemba.”

Sehemu nyingine inasomeka, “Hapo siku za nyuma Wapemba walidai kisiwa chao, na ninyi viongozi mkang’ang’ania kuwa hatuwezi kuvunja umoja. Sasa mnaona hao tayari wameanzisha chama cha kisiasa cha ‘Uamsho’ kwa kisingizio cha dini.”

Kipeperushi hicho pia kimedai kwamba, asili ya wananchi wa Pemba ni Wamakonde kutoka Msumbiji wakati wenyeji wa Unguja wana asili ya Wasegeju kutoka Bara, ndiyo maana wanautaka Muungano.

“Kila siku mnajenga Unguja bila ridhaa yetu, nani mtu wa Unguja aliyejenga Pemba? Mnajenga mpaka ndani ya vyanzo vya maji, tunasema tokeni na hameni mara moja,” inasisitiza sehemu ya vipeperushi hivyo.

Huku wakilaumu marekebisho ya Katiba ya Zanzibar na kuitisha kura ya maoni iliyounda Serikali ya Umoja wa Kitaifa, wamesema wanahitaji Katiba Mpya ya Zanzibar ili kufuta mfumo huo.
Vipeperushi hivyo pia vimelaumu kundi la Uamsho kwa ubaguzi kwa wananchi wanaotoka bara na kusema, kuwa hata Wapemba wako kwa wingi upande huo wa pili wa Muungano.
Wamesisitiza pia kutaka Muungano kati ya Unguja na Tanganyika bila ya kuihusisha Pemba na kusisitiza:,

“Tunasema tena, sisi watu wa Unguja tunataka Muungano wa Serikali mbili ya Unguja na Tanganyika bila ya kuwapo Pemba. Kuwapo kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar isiyokuwa ya Umoja wa Kitaifa. Rais wa Zanzibar awe ndiyo Makamu wa Rais wa Muungano.”

Kauli ya Nyerere
Mwaka 1995 akiwa katika Hoteli ya Kilimanjaro  (sasa Hyatt Regency Dar es Salaam) , Mwalimu Nyerere akielezea nyufa kuu tano zilizokuwa zikiikabili nchi huku wa kwanza ukiwa ni Muungano.
Mwalimu alionya, “Watu wazima wameuzungumza Muungano, kwamba tuuvunje au tuendelee. Mtu mwenye akili hawezi kufikiri Uzanzibari ni fahari: Hana akili. Nje ya Muungano kuna Wapemba na Waunguja. Mtamaliza kutengana na Watanganyika, halafu mara mtakuta kumbe sisi si Wazanzibari.”

“Mtajikuta kuna Wapemba na Waunguja. Wapemba watapata msukosuko kidogo alololo! Mtakuta kumbe kuna Wazanzibari na Wazanzibara. Hamtakaa salama. Hamuwezi mkakaa salama baada ya kutenda dhambi ya kuwabagua watu wa nchi yenu ileile moja mkawaita wale wao na hao sisi. Dhambi ile haishii hapo. Ndivyo historia ilivyo; ni sheria ya historia siyo sheria ya Mwalimu Nyerere.”

Kinyume na onyo hilo la mwalimu, vipeperushi hivyo vimeorodhesha madai mengine, mojawapo likiwa kwamba Rais wa Jamhuri ya Muungano awe anapatikana kwa zamu ya kipindi kimoja kila upande wa Muungano.

Pia kundi hilo limedai kuwa Waziri Mkuu atoke bara, kila upande uwe na rasilimali zake kama vile mafuta na madini, ulinzi wa nchi uwe wa pamoja, kuwe na mgawo sawa wa mabalozi nje ya nchi na kuwa na mgawanyo sawa wa misaada ya maendeleo.

Tamko la Jumiki
Kwa upande wake Msemaji wa kundi la Jumik, Sheikh Faridi Hadi Ahmad amekosoa vipeperushi hivyo akisema vimejaa uzushi.

Akizungumza na waandishi wa habari katika msikiti wa Mbuyuni mjini Zanzibar juzi, Sheikh Faridi alisema kundi hilo halina uhusiano na Upemba wala Uunguja.

“Hao ni wapuuzi na wazushi, kama wanataka Wapemba warudi kwao, basi wamwambie na Rais Ali Mohamed Shein naye aondoke, Yule si ni mwenyeji wa Pemba?” alihoji Sheikh Farid.

Alisema kundi hilo lilianzishwa kwa ushirikiano na wananchi kutoka Pemba na Unguja kwa malengo ya kueneza dini na masuala mengineyo.

Kuhusu kujihusisha na siasa, alisema kuwa Katiba ya Zanzibar na dini ya Kiislamu inaruhusu waumini wake kushiriki siasa.

“Katiba ya Zanzibar inasema kuwa kila mtu ana haki ya kushiriki kwenye uongozi wa nchi. Hata Mtume Muhammad (S.AW), alikuwa ni rais wa eneo lake na alikuwa kiongozi wa dini… Siasa ni neno la Kiarabu likiwa na maana ya uongozi na uongozi una mambo mengi. Kwa hiyo tuna haki kabisa ya kushiriki siasa,” alisema Sheikh Farid.

Katika hatua nyingine, kundi hilo limepinga hatua ya Jeshi la Polisi kuwakataza kufanya miahadhara kama kawaida yao.

Katika barua yao waliyomwandikia Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mjini Magharibi, Uamsho wamelaumu hatua ya jeshi hilo huku pia wakimlaumu Waziri wa Nchi Katika Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Mohamed Aboud wakisema kuwa hana mamlaka ya kuwazuia kufanya hivyo.

Wameipongeza hotuba ya Rais Ali Mohamed Shein wakisema kuwa, haikukataza mihadhara badala yake alisisitiza amani.

Kamati ya Bunge
Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama, Edward Lowassa amekemea vikali hali ya machafuko yaliyojitokeza hivi karibuni visiwani humo na kutamka kwamba amani ya nchi lazima ilindwe kwa gharama yoyote.

Lowassa, aliwapongeza Rais Jakaya Kikwete na Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohammed Shein kwa kukemea vitendo viovu vilivyofanywa na baadhi ya watu kisiwani humo pamoja na kulinda usalama wa taifa.

Akizungumza jana wakati wa harambee ya ujenzi wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Usharika wa Elerai, Lowassa alionya kwamba amani ya nchi haiwezi kuchewa na watu wachache.

“Amani ya nchi italindwa kwa gharama yoyote ile, hatuwezi kuona amani ya nchi tuliyonayo inachezewa na watu wachache wenye nia mbaya,” alionya Lowasa.

Source: Mwananchi

LOWASA: Hawaniwezi

 From: MWANANCHI
 
WAZIRI Mkuu aliyejiuzulu, Edward Lowassa amewapiga vijembe aliowaita maadui zake kisiasa wanaomchafua katika majukwaa mbalimbali akisema kuwa, hawamuwezi na hawamnyimi usingizi.

Lowassa akitambia maadui zake, kambi yake nayo imezidi kujizatiti baada ya mshirika wake kisiasa na Mbunge wa Bariadi Magharibi, Andrew Chenge amefanikiwa kukalia kiti cha Kamati ya Bunge ya Fedha na Uchumi hivyo kuzidi kuongeza nguvu kwenye bungeni.

Jana, akiwa mkoani Arusha katika harambee ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Usharika wa Elaira, Lowassa alitumia sehemu ya muda wake kuwapiga vijembe maadui zake pasipo kuwataja majina akisema kamwe hawamnyimi usingizi.
Lowassa ambaye pia ni Mbunge wa Monduli, alitoa kauli hiyo, baada ya Askofu wa Dayosisi ya Kaskazini Kati, Thomas Laizer kumtaka aendelee kufanya kazi ya Mungu licha ya baadhi ya watu kumkatisha tamaa.

Akizungumzia kauli ya Askofu Laizer, Lowasa alisema mahasimu wake kisiasa wamekuwa wakimsema kupitia vyombo mbalimbali vya habari, lakini akatamba kwamba juhudi hizo hazitaweza kufua dafu kwake kwani kelele zao hazimnyimi usingizi.

“Wanaonisema kwenye magazeti wala hawanisumbui, nasema hawaninyimi usingizi kwa kuwa mimi namtegemea yule anitiaye nguvu daima,” alisema Lowasa, kitendo kilichosababisha kushangiliwa na waumini waliohudhuria kanisani hapo.

Aliongeza kuwa yeye daima humtegemea Mungu amtiaye nguvu na kamwe hawezi kushindwa kulala usingizi kwa kusikiliza kelele zao za mara kwa mara.

“Nakushukuru Baba Askofu kwa kunijibia, wale wote wanaonisemasema kwenye magazeti wala hawanisumbui na wala hawaninyimi usingizi,” alisema Lowasa.

Alisema kwamba yeye ataendelea kumtumikia Mwenyezi Mungu ambaye amtiaye nguvu siku zote bila kujali maneno ya mahasimu wake wa kisiasa.
Kabla ya kuendesha harambee hiyo, Lowasa aliwaongoza waumini wa kanisa hilo kwa nyimbo zilizopo kwenye Kitabu cha Tenzi za Rohoni na kuibua shangwe kanisani hapo.

Kambi yake yajizatiti
Chenge ambaye ni mshirika mkubwa wa Lowassa kisiasa amechaguliwa katika kamati nyeti ya Bunge ya Fedha na Uchumi, akizidi kuongeza nguvu kwenye mhimili wa kambi hiyo.

Lowassa mwenyewe anaongoza Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama huku mshirika wake mwingine, Peter Serukamba akiongoza Kamati ya Miundombinu.

Katika uchaguzi wa juzi wa kamati hiyo uliotawaliwa na malalamiko ya vitendo vya rushwa bila kuelezwa ilikuwa ikitolewa na kambi ipi, aliyechaguliwa kuwa Makamu Mwenyekiti ni Dunstan Kitandula ambaye ni mbunge wa Mkinga.

Uchaguzi huo ulikuwa wa kujaza nafasi iliyoachwa wazi na Dk Abdallah Kigoda aliyeteuliwa kuwa Waziri wa Viwanda hivi karibuni.

Akizungumzia uchaguzi huo jana, Katibu wa Bunge, Dk Thomas Kashililah alisema, Chenge alipata nafasi hiyo baada ya kumshinda Mbunge wa Lupa, Victor Mwambalaswa.


“Mwambalaswa alikuwa Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Fedha na Uchumi kabla ya uchaguzi, hivyo aliamua kujiuzulu ili kugombea nafasi ya uenyekiti na Chenge, lakini akashindwa," alifafanua Dk Kashillilah.

Alipotakiwa kuzungumzia mizengwe na rushwa iliyotawala kwenye uchaguzi huo, Dk Kashililah alisema hawezi kuzungumzia hilo kwa sababu hakuwepo kwenye mchakato wa upigaji kura.

“Wanaoweza kuzungumzia hilo ni wale waliopiga kura ndiyo wanaweza kuelewa kama kulikuwa na mazingira ya rushwa lakini mimi sikuwapo,” alisema.

Tayari kambi ya Lowassa pia inaonekana kuwa na nguvu katika baadhi ya kamati kutokana na kuwa na washirika wenye msimamo wa wastani akiwemo Agustine Mrema wa Kamati ya Bunge ya Serikali za Mitaa (LAAC), Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali Kuu (PAC) inayoongozwa na John Cheyo, Kamati ya Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC) inayoongozwa na Zitto Kabwe na hata Kamati ya Bunge ya Katiba ya Sheria na Utawala inayoongozwa na Pindi Chana

Saturday, June 2, 2012

HOTUBA Ya Kikwete!


Ndugu Wananchi,

Kama ilivyo ada, namshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa Rehma, kwa kutujaalia uhai na kutuwezesha kumaliza mwezi Mei salama. Kwa kutumia utaratibu wetu wa kuzungumza kwa njia hii kila mwisho wa mwezi, leo nitazungumzia mambo matatu.

Mkutano wa G-8
Jambo la kwanza, ni suala la usalama wa chakula na lishe. Duniani, inakadiriwa kuwa kuna watu milioni 925 wanaokabiliwa na njaa na lishe duni. Kati ya hao Afrika ina watu milioni 239 ambao ni karibu theluthi moja ya watu wote wenye tatizo la njaa na lishe duni kote duniani.

Nchi za Afrika zenye tatizo la njaa kiasi cha kuhitaji msaada wa chakula kutoka nje ni 27. Kati ya hizo 11 zina matatizo makubwa zaidi. Tanzania siyo miongoni mwa nchi hizo, hata hivyo bado hatujafikia kiwango cha kujitosheleza kabisa. Hivi sasa tumefikia asilimia 95 na kila mwaka yapo maeneo nchini yanayopata msaada wa chakula kutoka Serikalini.

Mwaka 2009, katika mkutano wao wa L’Aquila, Italia, viongozi wa nchi nane tajiri kuliko zote duniani waliamua kuchukua hatua ya kuzisaidia nchi zinazoendelea duniani kukabiliana na tatizo la njaa na lishe duni. Katika mkutano ule waliahidi kutoa dola za Marekani bilioni 22 kwa ajili hiyo. Tanzania tunategemea kupata dola milioni 22.9.

Katika mkutano wa nchi hizo maarufu kwa jina la G-8 uliofanyika Camp David, Marekani tarehe 19 Mei, 2012, pamoja na mambo mengine walizungumzia suala la usalama wa chakula na lishe barani Afrika. Nia yao ni kuchangia katika juhudi zinazofanywa na mataifa ya Afrika zenye shabaha ya kutokomeza matatizo hayo. Tofauti na walivyofanya L’Aquila, safari hii waliamua kuchangia katika utekelezaji wa mipango na progamu za kuendeleza kilimo katika nchi za Afrika hasa zile zinazolenga
kujenga usalama wa chakula na lishe.

Aidha, waliamua kuwa wataanza na nchi tatu na kuendelea kuziongeza kila baada ya muda fulani, badala ya kuanza na nchi zote mara moja. Hoja yao kubwa ni kwamba, wanataka kukusanya nguvu zao kwa nchi hizo chache ili kufanya kazi ambayo itakuwa na matokeo yanayoonekana katika
kutokomeza njaa na kuboresha lishe. Hawakupenda kusambaza nguvu zao kwa nchi nyingi na kuishia kutokufanya kazi ya maana.


Ndugu wananchi;
Bahati nzuri katika programu na mipango ya nchi iliyokubaliwa kwa awamu ya kwanza ni Tanzania, Ethiopia na Ghana. Na, jambo la kufurahisha zaidi ni kwamba mpango wetu wa kuendeleza kilimo katika ukanda wa Kusini mwa Tanzania ulichukuliwa kuwa ni wa mfano. Maoni hayo ya nchi za G-8 ndiyo maoni ya WEF, Sekretariat ya NEPAD na Umoja wa Afrika, wote wameona kuwa mpango wetu unafaa kuenezwa barani Afrika kama mkakati sahihi wa kuendeleza kilimo, kujitosheleza kwa chakula na kupunguza umaskini.

Katika Bara la Afrika mkakati huo sasa unaitwa Grow Africa Partnership na tayari nchi saba zimeshajiunga nao. Nchi hizo ni Tanzania, Msumbiji, Kenya, Rwanda, Ethiopia, Ghana na Burkina Faso. Katika mkutano wa Camp David, nchi za Marekani, Japani, Uingereza, Ujerumani, Ufaransa na Urusi zimeahidi kuchangia nchi yetu katika juhudi zetu za kuendeleza kilimo na hasa zile zenye lengo la kujitosheleza kwa chakula na kuboresha lishe nchini. Ukichanganya na ahadi iliyotolewa na Umoja wa Ulaya katika mkutano huo, kiasi cha dola za Marekani milioni 897 zimeahidiwa kutolewa kwa nchi yetu kati ya sasa na mwaka 2015.

Ndugu Wananchi;
Mwaka 2006 tulizindua Programu Kabambe ya Kuendeleza Kilimo nchini maarufu kwa kifupi kama ASDP. Kwa kirefu kwa lugha ya Kiingereza ni the Agricultural Sector Development Programme. Programu hii ndiyo mwanzo wa safari yetu ya uhakika ya kuleta mapinduzi ya kilimo nchini
Tanzania. Jambo la kwanza lililofanyika katika utayarishaji wa Programu hii ni kutambua vikwazo vinavyozuia maendeleo ya kilimo nchini na kupendekeza hatua za kuchukua za kuondosha vikwazo hivyo.

Mwaka 2008, katika tathmini iliyofanywa kwa ushirikiano wa Serikali na Sekta Binafsi kwa uamuzi wa Baraza la Biashara Tanzania, ilidhihirika kwamba sekta binafsi ambayo ni wadau muhimu, haijahusishwa vya kutosha katika mikakati, mipango na programu za kuendeleza kilimo nchini. Kwa
pamoja ilikubaliwa kuwa kasoro hiyo iondolewe ili wadau wote washirikishwe, yaani Serikali, wakulima wadogo, wakulima wakubwa na sekta binafsi. Vilevile, sote tulikubaliana kutoa kipaumbele cha juu kwa maendeleo ya kilimo. Kwa pamoja tuliafikiana kuwa mambo mengine
yanaweza kusubiri isipokuwa kilimo. Matokeo ya maelewano hayo ndiyo yaliyozaa mkakati na kauli mbiu ya “Kilimo Kwanza”.

Ndugu Wananchi;
Tangu wakati huo, sekta binafsi nchini imekuwa inahusishwa na kushirikishwa kwa ka ribu katika utekelezajiwa ASDP na kuendeleza kilimo kwa jumla. Kwa upande mmoja sekta binafsi imekuwa inahusishwa katika upatikanaji wa zana na pembejeo za kisasa za kilimo kwa wakulima. Kwa ajili hiyo, wenzetu wa sekta binafsi wamekuwa wanategemewa kuleta na kuuza matrekta, mitambo na vifaa mbalimbali vya kilimo pamoja na mbegu, mbolea, dawa za kuua wadudu waharibifu wa
mazao na za kukinga na kutibu maradhi ya mimea na mifugo. Hali kadhalika, wamekuwa wanajihusisha na ununuzi na usindikaji wa mazao ya mkulima na kuongeza thamani. Tunataka tuachane na kuendelea kuuza nje mazao ya kilimo kama malighafi na kununua bidhaa zilizotengenezwa na mazao hayo.

Upande mwingine tuliwategemea wenzetu wa sekta binafsi washiriki kulima mashamba makubwa. Wasiache kazi ya kilimo kufanywa na wakulima wadogo peke yao ambao uwezo wao si mkubwa wa kukabili matatizo ya kuongeza tija. Nafurahi kwamba wito wangu huo waliupokea vizuri na
baadhi yao wameshaanza kufanya hivyo.

Ndugu Wananchi;
Swali kubwa walilouliza ndugu zetu hao siku ile ya tarehe 2 – 3 Juni, 2009 pale Kunduchi Beach Hotel ni kuhusu upatikanaji wa ardhi. Niliwaeleza kuwa upo utaratibu mzuri wa kuwapatia wakulima wakubwa ardhi ya kilimo na ufugaji. Utaratibu wenyewe ni kwamba kila wilaya imetakiwa kutenga ardhi kwa ajili ya wakulima wakubwa. Hilo likishafanyika, taarifa hutolewa kwa Kituo cha Uwekezaji na kuingizwa katika kitu kinachoitwa Benki ya Ardhi. Mwekezaji anapojitokeza,
kulingana na aina ya kilimo anachotaka kujihusisha nacho, hugawiwa ardhi hiyo. Ardhi hiyo ni ile ambayo siyo inayotumiwa na wakulima wadogo. Katu hawanyang’anywi ardhi wakulima wadogo ili kuwapa wakulima wakubwa. Hiyo siyo sera wala madhumuni na malengo ya ASDP au Kilimo
Kwanza. Nalifafanua hili kuondoa hofu iliyokuwepo na upotoshaji uliokuwa unafanywa makusudi wa kuhusisha wakulima wakubwa na uporaji wa ardhi. Siyo makusudio yake hata kidogo.

Ndugu Wananchi;
Mwaka 2010 tukapanua wigo wa ushiriki wa sekta binafsi kwa kuihusisha sekta binafsi ya kutoka nje ya nchi. Mwaka huo pia, tukaamua kuipa sekta binafsi lengo maalum la kutekeleza nalo ni kushiriki katika kilimo cha kuhakikisha kuwa nchi yetu inajitosheleza kwa chakula na kupata ziada kubwa ya kuuza nje, kwa majirani zetu na kwingineko. Shabaha yetu hasa ilikuwa ni kujitosheleza kwa vyakula vikuu vya mahindi, mchele na sukari.

Aidha, tuliamua pia kuwa, kwa kuanzia tuelekeze nguvu zetu kwenye mikoa ya Rukwa, Mbeya, Ruvuma, Iringa na Morogoro kwa vile mikoa hiyo ndiyo ghala la chakula la nchi yetu. Kwa vile mikoa hiyo ipo ukanda wa kusini ndio maana ikaja kuitwa Southern Agriculture Growth Corridor of
Tanzania au SAGCOT. Tumeamua tukusanye nguvu za Serikali, wakulima, sekta binafsi na washirika wetu wa maendeleo kuwekeza katika kuendeleza kilimo katika mikoa hiyo.

Ndugu Wananchi;
Utekelezaji wa mpango wa kuendeleza kilimo katika ukanda wa SAGCOT una shabaha kuu mbili: Kwanza kabisa mpango unalenga kuboresha kilimo cha wakulima wadogo ili kitoke kuwa duni na cha kujikimu na kuwa cha kisasa na kibiashara. Chini ya mpango huu wakulima wadogo watasaidiwa
na kuwezeshwa kupata na kutumia zana na pembejeo za kisasa za kilimo. Pia watawezeshwa kupata mikopo kwa ajili ya kilimo na masoko ya uhakika na yenye bei nzuri kwa mazao yao. Vile vile, huduma muhimu zitaimarishwa. Hapa tunazungumzia maafisa ugani na miundombinu ya
umwagiliaji, barabara, umeme, maji safi na teknolojia ya habari na mawasiliano.

Pili, kwa pale inapowezekana kwa maana ya upatikanaji wa ardhi na aina ya mazao, kuihusisha sekta binafsi katika kilimo. Tayari utekelezaji wa mpango wa SAGCOT umeanza. Kamati ya Utendaji imeshaundwa na Sekretariati yake imeshateuliwa. Aidha, Mfuko wa Kuchochea Uwekezaji
umeshaanzishwa na unaendelea kuchangiwa fedha.

Ndugu Wananchi;
Utekelezaji wa malengo ya SAGCOT kwa kilimo cha mpunga na kuongeza uzalishaji wa sukari yameanza kutekelezwa. Matayarisho yanaendelea kwa kilimo cha mahindi na mazao mengine.

Mpango huu utakapofanikiwa utakuwa na manufaa makubwa. Nchi yetu itajitosheleza kwa chakula na kuwa na ziada kubwa ya kuuza nje. Inakadiriwa kuwa mapato yatokanayo na kilimo katika ukanda huu yatafikia dola bilioni 1.2 kwa mwaka, watu 420,000 watapata ajira na watu 2,000,000 wataondokana na umaskini uliokithiri.

Uwekezaji wake ni mkubwa na kwamba kiasi cha dola bilioni 3.4 kinahitajika kwa kipindi cha miaka 20. Kwa ushirikiano uliopo baina ya Serikali, sekta binafsi na wabia wetu wa maendeleo wakiwemo wa nchi za G-8, hayo yote yanawezekana.

Ndugu Wananchi;
Tukijitosheleza kwa chakula na kwa maana pana ya chakula chenye lishe bora tutakuwa tumefanikiwa kupata ufumbuzi wa tatizo kubwa la ukosefu wa lishe bora miongoni mwa wananchi wa Tanzania. Wanaoathirika sana na tatizo hili ni kina mama wajawazito na watoto wenye umri wa chini ya miaka mitano. Ukosefu wa lishe bora huchangia asilimia 20 ya vifo vya kinamama wajawazito nchini na theluthi moja ya watoto wa umri wa chini ya miaka mitano. Aidha, asilimia 42 ya watoto wa umri wa chini ya miaka mitano wamedumaa na asilimia 16 wana uzito mdogo kulingana na umri wao na asilimia 59 wana upungufu wa damu. Kwa kina mama wajawazito asilimia 41 wana matatizo ya upungufu wa damu. Hali hii sio nzuri hata kidogo lazima tuibadili na tunaweza kufanya hivyo. Tunao mkakati wa kitaifa wa kuboresha lishe ambao kwa sehemu kubwa utanufaika sana na kufanikiwa kwa mkakati wa kujitosheleza kwa chakula.

Mkutano wa Benki ya Maendeleo ya Afrika
Ndugu Wananchi;
Jana tarehe 31 Mei, 2012 nilishiriki katika sherehe za ufunguzi wa Mkutano wa 47 wa Bodi ya Magavana wa Benki ya Maendeleo ya Afrika na Mkutano wa 38 wa Mfuko wa Maendeleo wa Afrika. Hii ni mara ya kwanza katika historia ya Benki hii tangu ianzishwe mwaka 1964 kwa nchi yetu kuwa mwenyeji wa mikutano hii inayofanyika kila mwaka. Ni heshima kubwa sana kwa nchi yetu, nami kwa niaba ya Watanzania wenzangu wote, nimemshukuru sana Rais wa Benki hiyo, Dkt. Donald Kaberuka kwa ihsani kubwa aliyoifanyia nchi yetu.

Kuwa mwenyeji wa mkutano mkubwa kama huu ni jambo lenye manufaa mengi kwetu. Kwanza husaidia kuitangaza nchi yetu Barani Afrika na kwingineko duniani. Pili, ni fursa nzuri ya kuzungumza na viongozi wa Benki kuhusu mipango na miradi yetu ya maendeleo tunayohitaji msaada kutoka Benki hiyo.

Na, tatu, ni fursa nzuri ya watu wetu kufanya biashara. Mkutano huu umeshirikisha watu 2,500 ambao wametoka nje ya Tanzania na wanajitegemea kwa kila kitu. Wenye hoteli, migahawa, vyombo vya usafiri, huduma ya simu, internet na nyinginezo watakuwa wamefanya biashara nzuri katika wiki nzima kabla ya tarehe 28 Mei mkutano ulipoanza hadi 2 Juni, mkutano utakapofungwa. Ni kutokana na manufaa kama haya, ndio maana huwa tunahangaika kuvutia mikutano mikubwa kuja
kufanyikia hapa nchini.

Ndugu Wananchi;
Napenda kutumia nafasi hii kutoa pongezi na shukrani nyingi kwa ndugu zetu wa Arusha kwa kuwapokea vizuri na kuwakarimu vyema wageni wetu hao. Nawaomba waendelee na moyo huo mpaka watakapoondoka wote. Naomba kuwepo kwa mkutano huu kuwakumbushe umuhimu wa mji wenu kuwa tulivu. Miaka miwili iliyopita isingekuwa rahisi kwa watu au shirika kubwa la
kimataifa kama Benki hii kuamua kufanya mkutano wake Arusha. Isitoshe hata sisi wenyewe tusingeshawishika kuomba au kukubali maombi ya namna hiyo. Lakini sasa imewezekana. Naomba kila mmoja wetu aweke azimio moyoni mwake la kuhakikisha kuwa hali ile haijirudii tena. Nyota ya
Geneva ya Afrika lazima iendelee kuangaza. Yaliyopita si ndwele tugange yajayo.

Watanzania Wenzangu;
Niruhusuni tena niwashukuru wenzetu wa Benki ya Maendeleo ya Afrika kwa mchango mkubwa waliotoa na wanaoendelea kutoa kuchangia maendeleo ya nchi yetu. Kwa miaka mingi Benki hii imekuwa inatupatia mikopo na misaada muhimu kwa maendeleo ya sekta mbalimbali nchini pamoja na zile za elimu, afya, maji na miundombinu ya barabara, reli, umeme n.k.

Kwa msaada wa Benki hii tunajenga barabara ya Namanga – Arusha, Minjingu – Singida, Namtumbo – Tunduru, Iringa – Dodoma, Mayamaya – Babati, na Tunduru – Mangaka – Mtambaswala. Miaka ya nyuma pia walituwezesha kujenga barabara ya Mutukula – Muhutwe. Aidha, hivi sasa wanagharamia upembuzi yakinifu na usanifu wa reli mpya tunayotaka kuijenga kutoka Dar es Salaam hadi Rwanda na Burundi.

Matukio ya Uvunjifu wa Amani Zanzibar
Ndugu Wananchi;
Jambo la tatu ninalotaka kuzungumza nanyi leo ni matukio ya wiki iliyopita huko kwenye Jiji la Zanzibar katika mkoa wa Mjini Magharibi, Unguja. Kama tujuavyo sote kulitokea ghasia zilizochochewa na viongozi wa Jumuiya ya Uamsho na Mihadhara ya Kiislamu maarufu kwa jina la
Uamsho. Taasisi hii imeanzishwa kwa madhumuni ya kidini, lakini hivi sasa viongozi wake wameamua kuyaacha madhumuni hayo na kubeba ajenda za siasa.

Siku za nyuma, ndugu zetu hawa walikuwa wakitumia muda mwingi kuilaumu Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. Baada ya kuundwa kwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa lawama hizo sasa hazisikiki. Lakini, mara tulipoanzisha mchakato wa kutengeneza Katiba mpya ya Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, mihadhara yao imeelekezwa kupinga Muungano na kuwakashifu viongozi waasisi wa Muungano na hata waliopo sasa. Isitoshe wamekuwa wakipandikiza chuki dhidi ya ndugu zao wa kutoka Tanzania Bara na wale wafuasi wa dini ya Kikristo.

Baya zaidi, katika uchochezi huo majengo na mali za Makanisa mawilizilichomwa moto, maduka ya watu kuvunjwa na mali zao kuibiwa. Kwa kweli vitendo hivi ni uhalifu ambao haukubaliki na wala hauvumiliki. Naungana na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein kwa kauli yake aliyoitoa jana katika mkutano wake na waandishi wa habari ya kukemea vikali na kulaaniuhalifu huo.

Ndugu Wananchi;
Ni jambo la kusikitisha na kushangaza kwamba, wenzetu hawa wamefanya uhalifu huo kwa hoja ya kupinga Muungano. Haiwezekani mtu anayepinga Muungano, akaitetea hoja yake kwa kuchoma moto makanisa au kuvunja maduka ya watu na kupora mali zao. Ukristo haukuingizwa Zanzibar na
Muungano, bali ulikuwepo karne kadhaa kabla ya Muungano na wala haukutokea Tanzania Bara. Na kama alivyoeleza Mheshimiwa Rais Ali Mohamed Shein jana, ukweli ni kwamba, dini ya Kikristo kama ilivyo ya Kiislamu imeenezwa Bara kutokea Zanzibar. Kanisa kuu la Anglikan Zanzibar lilijengwa kuanzia mwaka 1873 na lile la Katoliki kuanzia 1893 ni miongoni mwa Makanisa makongwe kuliko mengi kama siyo yote kwa upande wa Zanzibar na Bara.

Katika hotuba yake ya jana, Mheshimiwa Rais, Dkt. Ali Mohamed Shein,pamoja na kueleza kwa ufasaha ukweli huu, pia alisisitiza suala la haki na uhuru wa Kikatiba wa mtu kuchagua au kubadilisha dini au imani yake. Katika kutumia uhuru huo, mtu hastahili kuingiliwa au kulazimishwa na mtu yo yote. Hayo pia ndiyo matakwa ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa kweli yanayofanywa na ndugu zetu wa Uamsho ya kuchoma moto makanisa siyo sawa hata kidogo. Na, wanapoyafanya kwa kisingizio cha Muungano ni jambo lisiloeleweka kabisa na wala halina mantiki. Labda wenzetu wana lao jambo.

Ndugu Wananchi;
Jambo lingine la kushangaza zaidi ni kule kutokea vurugu na ghasia hizi dhidi ya Muungano wakati ambapo Serikali imetoa fursa sasa kwa watu kutoa maoni yao kwenye mjadala wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano. Kama tujuavyo sote, Tume ya Katiba imekwishaundwa na inajiandaa kupita
kote nchini kukusanya maoni ya wananchi juu ya Katiba mpya waitakayo. Kama mtu ana maoni yake kuhusu Muungano, hiyo ndiyo fursa ya kufanya hivyo. Utaratibu mzuri umewekwa kwa ajili yetu sote, vurugu za nini?

Ndugu Zangu, Watanzania Wenzangu;
Mimi sioni sababu ya msingi ya kusababisha kuvurugika kwa amani kwa jambo ambalo limewekewa utaratibu muafaka wa kulishughulikia. Nawaomba tutumie utaratibu mzuri uliowekwa badala ya kufanya mambo yanayoleta mifarakano katika jamii na yanayosababisha uvunjifu wa amani na
yanaharibu sifa na sura ya Wazanzibari na Watanzania isivyostahili.

Ndugu zangu,
Haipendezi wala haifurahishi kwa Serikali kuchukua hatua kali dhidi ya raia wake. Lakini, kama hapana budi, Serikali lazima ifanye na haitasita kufanya hivyo. Narudia kuwasihi viongozi na wafuasi waJumuiya ya Uamsho kurejea kwenye madhumuni ya msingi ya jumuiya yao. Wajiepushe na ajenda za kisiasa na kupandikiza chuki zitakazosababisha mifarakano baina ya wananchi wa pande zetu mbili za Muungano na baina ya Wakristo na Waislamu. Watanzania ni ndugu na wamekuwa wanaishi pamoja kwa upendo na furaha licha ya tofauti zao za rangi, makabila,
dini na maeneo watokako. Kimeharibika kipi hata leo yatokee haya? Aidha nawaomba wenye maoni kuhusu Muungano wetu, muundo wake na uendeshaji wake watumie fursa ya mjadala wa Katiba kutoa maoni yao. Huhitaji kufanya ghasia kutoa maoni yako!

Ndugu Wananchi;
Napenda kutumia fursa hii pia kuwapa pole wale wote walioathirika na vurugu zilizotokea. Nawaomba wawe wastahamilivu, hiyo ndiyo mitihani ya maisha. Serikali zetu mbili zitafanya kila lililo kwenye mamlaka yake kuwahakikishia wananchi wote usalama wa maisha yao na wa mali
zao.

Nawapongeza vijana wetu wa Jeshi la Polisi kwa juhudi kubwa waliyoifanya ya kudhibiti hali ambayo mwelekeo wake haukuwa mwema. Nawaomba waendelee kuwa macho ili watu wasioitakia mema nchi yetu na watu wake wasipate nafasi ya kutuvurugia amani na utulivu wetu. Naamini tukidumisha utamaduni wetu wa kuheshimiana, kuvumiliana na kuzungumza pale tunapotofautiana hakuna litakaloharibika. Haya shime tufanye hayo.


Mungu Ibariki Afrika!
Mungu Ibariki Tanzania!
Asanteni kwa Kunisikiliza.

Thursday, May 31, 2012

"NAPE Ni GAMBA Linalotakiwa Kuvuliwa!" - MAIGE


Akizindua matawi mawili ya wakereketwa wajasiriamali wa CCM katika Kijiji cha Isaka, Kahama, Shinyanga, Maige ambaye ni Mbunge wa Msalala alimtaka Nape kuacha tabia yake ya kutoa kauli ambazo kwa namna moja au nyingine zinaelekea kukidhoofisha chama.

Alimtaka kupima utendaji wake tangu alipoishika nafasi hiyo ya Itikadi na Uenezi na kujiuliza ni wanachama wangapi wameingia ndani ya chama hicho.

Alisema sasa hivi kuna wimbi kubwa la wanachama wa chama hicho kuhama na kukimbilia upinzani na kusema ni wajibu wa Nape kupima na kuona kuwa kazi ya itikadi na uenezi haiwezi na kwani hajui wajibu wake akisema ni mtu wa kumhurumia.

Maige alisema mbali ya kushindwa kuzuia wimbi la wanachama kukihama CCM pia hapaswi kuvumiliwa kutokana na kauli yake kwamba hata kama wanachama watahama wote na akabaki yeye (Nape) peke yake, haitakufa. Alisema kauli hiyo haikijengi chama, bali kuchochea makundi ambayo yanaweza kukibomoa.

Alisema akiwa mwana CCM anaona kwamba sasa hivi Nape amekuwa hafanyi kazi ya uenezi na kukirejeshea haiba na mvuto ambao umepotea kwa wananchi na kwamba, kazi anayoifanya sasa ni kukuza makundi na kusema ovyo.

Aliendelea kumshambulia Nape kwa maneno akisema amejenga jeuri, kiburi, dharau na ulevi wa madaraka huku akidai kwamba kitendo cha CCM kupoteza wanachama zaidi ya 10,000 kwa wakati mmoja mkoani Arusha na sehemu nyingine wanachama 3,000 ni ishara ya hatari lakini, Nape amekuwa akiwaita wanaohama kwamba ni mzigo.

“Huyu Nape ni lazima atupishe. amekifanya chama kama mali yake, yeye ndiye mwenye jukumu la kueneza sera za chama na kutafuta wanachama wapya, lakini ndiyo kwanza anasema waachwe waondoke, Chadema wanatamba kila siku yeye hajali, huyu nasema ni gamba ni bora atupishe,” alisema.

Baada ya mashambulizi hayo, Maige alijitetea kwamba maneno yake dhidi ya Nape yasitafsiriwe kama ni kuulilia uwaziri: “Ni uchungu nilionao kwa chama changu kuona kila siku zinavyokwenda ndivyo tunavyopoteza idadi kubwa ya wanachama, tuliyemkabidhi jukumu la uenezi anasema hajali, sasa huyu si atupishe mapema kabla mambo hayajaharibika?”

“Nikuombe Mwenyekiti wa CCM Mkoa mzee wangu, Mgeja (Hamis), nafikiri ninyi wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (Nec ya CCM) mnapaswa kuchukua hatua haraka juu ya Nape... huyu sasa ni tatizo. Chama kitawafia hivihivi mkiona, avuliwe gamba maana tukisubiri ajivue atatuchelewesha, CCM ni wanachama si Nape.”

Wakati Maige akitoa maneno hayo, Mgeja alikuwa ameinamisha kichwa chake chini huku mikono ikiwa kichwani, lakini wana CCM na wananchi wengine walikuwa wakishangilia.

Aidha, Maige aliwalaumu viongozi wa CCM katika ngazi ya wilaya na kata ambao wamekuwa na tabia ya kutowatembelea wananchi katika maeneo yao kusikiliza kero zao wakisubiri mpaka viongozi wa kitaifa ndipo na wao wajitokeze.

“Jamani inakuwaje kiongozi mwenezi wa CCM kata ama wilaya anakaa kimya kabisa hakuna kazi yoyote anayoifanya! Viongozi wa aina hii wasipewe nafasi kabisa katika uchaguzi ujao. Tupate safu ya viongozi wenye kukifia chama chetu.”

“Maana kama watu wanakuja na Operesheni Sangara hakuna anayesimama kujibu, Operesheni Vua Gamba Vaa Gwanda hakuna aliyewajibu wala CCM haijatafuta operesheni yoyote ile kukabiliana nao, sasa wameanza Operesheni Movement For Change (M4C), sisi na Nape wetu kimya tunawaangalia tu wanazoa wanachama. Tuwe makini chagueni viongozi wenye uchungu na chama,” alisema Maige.

Alipotakiwa kuzungumzia tuhuma hizo za Maige, Nape alisema: “Nasubiri taarifa rasmi ya chama na nikiyakuta hayo nitajibu. CCM ina taratibu zake katika utendaji wake wa kazi. Katika taratibu hizo, ziara zote za viongozi wetu zinaandikiwa taarifa ambayo lazima zipite kwangu. Hayo unayosema yakinifikia, nitayajibu lakini siwezi kuzungumza bila hakika kwamba amesema.”

Bonyeza Hapa Ilikusoma Makala Inayozungumzia Utendaji wa Nape katika Nafasi aliyonayo Na Jinsi ambavyo unaweza kukiponza Chama cha Mapinduzi

Taarifa hii ni sehemu ya Taarifa ya Gazeti la Mwananchi, May 31 2012!

Wednesday, May 30, 2012

UDINI: TAMKO la WAISLAMU Dhidi ya WAKRISTO!

 Utangulizi
Oktoba 31, 2010 Tanzania ilifanya uchaguzi mkuu ambapo wananchi walipata fursa ya kumchagua Rais, wabunge pamoja na madiwani. Katika uchaguzi huo, Watanzania kwa ujumla wao walikichagua Chama cha Mapinduzi, CCM, kuongoza tena nchi kwa kipindi kingine cha miaka mitano.

Hata hivyo, wakati wananchi wakiamini kwamba wanaongozwa na watu waliowapigia kura, matukio yanayoendelea hivi sasa yanaashiria serikali kutelekeza majukumu yake na kuwaacha maaskofu wakielekeza nchi wanakotaka.

Itakumbukwa kwamba awali kabla ya uchaguzi mkuu maaskofu walikuwa wametoa Ilani yao ya uchaguzi bila kueleza kipi chama chao kitakachosimamia na kutekeleza Ilani hiyo. Baadhi ya viongozi wa serikali na chama tawala, CCM, walishabikia Ilani hiyo na kuwatetea maaskofu. Kwa hakika taarifa za vyombo vya habari zilifahamisha kwamba baadhi ya watendaji waandamizi ndani ya serikali walishiriki katika kuandaa Ilani hiyo.

Ilipofika wakati wa kampeni hadi kuingia siku ya kupiga kura, ilikuwa imedhihiri kipi kilikuwa chama cha maaskofu ambacho walitarajia kitekeleze Ilani yao. Haikuwa tena jambo la siri kwani walisimama wazi wazi kuwaelekeza waumini wao wampigie nani kura. Na katika juhudi zao za kutaka wafuasi wao wawaelewe vizuri, maaskofu walithubutu hata kuweka kando mafundisho ya Biblia yao juu ya masuala ya uzinzi wakawahimiza waumini kumpigia kura mtu wanayemtaka bila kujali kwamba anakabiliwa na kashfa ya kupora mke wa mtu. Waliwaambia wasihangaike na maisha binafsi ya ndoa ya mgombea.
 
Hata hivyo, matokeo ya kura yalitoa majibu kwamba Watanzania walikuwa wameikataa Ilani ya Maaskofu.

Waislamu tumelazimika kukutana na kutoa tamko hili kwa sababu matukio yanayotokea hivi sasa yanaonesha kuwa wale ambao Watanzania walikataa kuwapa uongozi na Ilani yao iliyoandaliwa na maaskofu, ndio sasa wanaielekeza nchi pa kwenda huku viongozi wa CCM na serikali wakijitahidi kadiri ya uwezo wao kunyenyekea kwa maaskofu hao.

Tumeona na tumemsikia Waziri Mkuu Mheshimiwa Mizengo Kayanza Peter Pinda akihangaika kuwapigia magoti na kuwaomba radhi maaskofu kule Sumbawanga. Tumesikia jinsi viongozi wanaojaribu kuwaambia maaskofu kwamba kama wanataka kuingia katika siasa wavue majoho na vyeo vyao vya kikanisa kama Padiri mwenzao waliyekuwa wakimpigania kuingia Ikulu, wanavyokemewa na kutakiwa wawaombe radhi maaskofu hao.
 

Lililo baya zaidi maaskofu walioshindwa kuwashawishi wananchi waipokee na kukubali Ilani yao, wamekuja na kampeni za kuchochea uasi kwa serikali iliyopo madarakani. Lakini pamoja na hali hiyo, viongozi wa CCM na serikali wamebaki wanagwaya. Hakuna aliyeweza kupata ujasiri wa kukemea hali hii. Kinyume chake Waziri Mkuu na Mzee John Samwel Malecela wanahangaika huku na kule wakiwapigia magoti maaskofu hao na kuwakemea wanaothubutu kuwakosoa.

Hali kama hii ni hatari kwa usalama na utulivu wa nchi. Ni hali ya kuchochea udini na kuweka ombwe la uongozi wa kisiasa ambao utazua balaa. Waislamu hatuwezi kukubali hali hii. Kwa hiyo, ama CCM na serikali vitekeleze wajibu wao wa kuongoza au kama wanaona hawawezi, basi waseme rasmi ili Maaskofu na wengine wenye Ilani zao za uchaguzi waingie tena ulingoni kuomba ridhaa ya Watanzania kuongoza nchi kuliko kuishi katika hiki kiini macho ambapo maaskofu na mawakala wao ndani ya serikali wameachwa waikokote nchi wanakotaka.
 

Kiini cha Hali hii ya Kisiasa
Hali hii ya kisiasa tunayoishuhudia leo nchini mwetu ni matunda ya mbegu liliyopandwa na kupaliliwa kwa zaidi ya miaka 100 iliyopita. Wakoloni walikuwa na kanuni yao waliyoiita divide et impero yaani wagawe ili uwatawale. Huko Rwanda wakoloni waliwagawa wananchi kwa misingi ya kikabila. Watusi ambao ni watawala wapewe elimu ya juu na wanfundishwe kwa Kifaransa, na Wahutu ambao ni watawaliwa wapewe elimu duni na wafundishwe kwa Kiswahili. Ubaguzi huo wa kuwagawa raia wa nchi moja ulipandikiza sumu iliyokuja kusababisha Wanyarwanda kuuana.

Hapa kwetu wakoloni walitugawa kwa misingi ya dini. Kabla ya uhuru wa Tanganyika, wakoloni kwa kushirikiana na makanisa waliwaona Waislamu kama ni mahasimu wao kidini na kisiasa. Na kwa sababu hiyo serikali za kikoloni zikaweka mikakati maalum ya kuwakandamiza Waislamu katika maeneo matatu: kwanza kuwawekea vikwazo katika kutangaza dini yao ili wasiongezeke; pili kuwabana katika elimu na ili kuhakikisha kuwa Waislamu wanabanwa jukumu la kuwaelimisha Waafrika likawekwa mikononi mwa makanisa na kazi ya serikali ni kuzigharimia tu shule hizo. Lengo likiwa ni kuwabatiza Waislamu wachache watakaoruhusiwa kusoma, na tatu kuwabana katika ajira serikalini kwa sababu makanisa yote yalisisitiza kuwa kuwaajiri Waislamu serikalini ni kusaidia kuenea kwa Uislamu..
 

Kwa kuwa ubaguzi huo haukuwa na kificho chochote, Waislamu wengi walijitokeza kupambana na ukoloni kwa matarajio kuwa serikali huru itaondosha chuki na uadui huo dhidi ya Waislamu. Lakini msiba mkuu wa taifa hili ni kwamba kinyume chake, baada ya uhuru msimamo ukawa ni ule ule wa kuwaona Waislamu kuwa ni maadui wa kupigwa vita na mikakati ya kuwabana Waislamu katika maeneo yale matatu ikaimarishwa zaidi wakati wa utawala wa Nyerere. Kuanzia 1957 mkakati uliopangwa na Kanisa Katoliki ukawa ni kuhakikisha kuwa nafasi zote muhimu za uongozi na serikali zinashikwa na wao. [Taz. Confidential Diary – Tanganyika, March-April 1957, uk. 3-4 Maryknoll Central Archives, New York ]. 

Na ni mkakati huu ndio ambao Mwalimu Nyerere aliokuwa akimuhakikishia Askofu Rweyemamu mwaka 1970 kuwa anatumia mamlaka yake kama Rais na kama kiongozi wa TANU kuhakikisha kuwa anatoa upendeleo maalum kwa Wakristo ili wasimamie sera za Chama. Na kwamba amemteua padiri katika nafasi nyeti ya Chama si kwa sababu anajua siasa bali kwa sababu ni Mkristo safi. Lakini Nyerere huyo huyo akisimama hadharani alijidai kukemea udini. Na kwa kazi kubwa aliyoifanya ya kuliimarisha kanisa na kuwadhoofisha Waislamu, leo Kanisa lake limo katika mchakato wa kumtangaza Nyerere kuwa ni Mtakatifu!
 
Sivalon anaarifu katika kitabu chake kuwa mara baada ya uhuru Kanisa katoliki liliwahamasisha Wakristo wote na hasa watendaji wa serikali juu ya hatari ya Ukomunisti na Uislamu na walikusanya nguvu zao zote katika kukabiliana na maadui hao.

Matokeo ya Hujuma Hizo
Matokeo ya hujuma hizo za kichinichini ni kwamba katika sura ya nje na katika propaganda za kisiasa Tanzania ni nchi moja yenye mshikamano na umoja na kisiwa cha amani. Lakini uhalisia wa mambo ni kuwa Tanzania ni nchi yenye jamii kubwa mbili. Jamii ya Wakristo wanaopewa msaada, upendeleo, ulinzi na heshima, na jamii ya Waislamu ambao wanachukiwa, kudharauliwa na kudhoofishwa na serikali kabla na baada ya Uhuru.



Maazimio ya Waislamu
Kwa kuzingatia muktadha wa hali ya kisiasa ilipofikia hivi sasa, Waislamu tumefikia maamuzi yafuatayo:

(1) Maadam Mfumo Kristo umeimarika kiasi cha kuweza kuitisha serikali na viongozi wake na wakatishika, na maadam Mfumo huo Kristo una nguvu za kuweza hata kuvitisha na kuvikemea vyombo vya dola na vikasalimu amri, Waislamu tutake tusitake, kama alivyohadharisha Mh. Membe, ukweli unabaki kuwa hautapita muda mrefu, dhulma hii ya udini italisambaratisha Taifa letu, kama udini ulivyoisambaratisha Ivory Coast ambayo katika miaka ya 1960 na 1970 ilikuwa mfano wa kuigwa.

Hivyo basi wajibu wetu wa mwanzo ni kuufikisha ujumbe huu kwa Waislamu wote nchini, na kuwataka wazingatie kuwa kwa kuwa wanabaguliwa na kudhalilishwa katika nchi hii kwa sababu ya Uislamu wao, basi ni wajibu wao na wao kushikamana kama Waislamu.
 

(2) Kwa kuwa kila wanchosema Maaskofu ndicho kinachofuatwa na serikali, na kwa kuwa Maaskofu wamekwishatamka hadharani na kwa sauti kali kuwa katika nchi yetu hakuna kabisa udini na atakayesema kuna udini basi ni yeye ndiye anayetaka kuleta udini, na kauli hiyo kudakwa na mawakala wa Maaskofu katika serikali, ni dhahiri kuwa dhulma za udini zinazoendelea kuwakandamiza Waislamu miaka 50 baada ya Uhuru hazitaondoshwa na Katiba mpya. Hivyo wajibu wetu mwingine ni kupigania ukombozi wa Waislamu ili washiriki katika kuandaa katiba mpya wakiwa ni raia huru na sawa na wenzao. Waislamu popote tulipo tunao wajibu wa kuorodhesha dhulma zote za udini tunazofanyiwa na kupigania ziondolewe kwanza na kulipwa fidia.

(3) Kwa kuwa tangu ukoloni hadi leo Waislamu wanahesabiwa na serikali na Maaskofu kuwa ni maadui wa kupigwa vita na wasiostahiki haki sawa na wengine, na kwa kuwa Waislamu wameazimia kutokukubali tena kudhulumiwa na kuonewa kwa namna yoyote ile iwayo, ni wazi kuwa hakuwezi kuwa na katiba itakayoweza kulinda haki za madhalimu na wadhulumiwa kwa wakati mmoja. Ingawa kwa propaganda za kisiasa Tanzania ni nchi moja, lakini kiuhalisia ni nchi yenye jamii mbili zenye hadhi na haki tofauti kabisa. 


Umefika sasa wakati wa kugawana nchi ili Waislamu wanaochukiwa na kunyimwa fursa sawa na Wakristo waishi katika maeneo yenye Waislamu wengi na Wakristo waishi katika maeneo yenye Wakristo wengi. 

Mwalimu Nyerere alipigania kwa nguvu zake zote Nigeria igawanywe ili Wakatoliki ambao walikuwa wanadhulumiwa Nigeria wajitenge na waruhusiwe kuishi katika nchi ya Biafra. Na katika kijitabu alichokiandika 1966 Nyerere alisema madai ya kuhifadhi umoja wa kitaifa wa Nigeria hayana maana yoyote pale ambapo baadhi ya raia wa taifa hilo wanadhulumiwa. Ushahidi wa dhulma za Waislamu upo wazi. Kugawana nchi kutawawezesha Waislamu kuwa na Mahakama ya Kadhi na kujiunga na OIC bila ya kuwakera Maaskofu. Ni wajibu wetu kulifikisha hili kwa Waislamu wenzetu nchi nzima ili lijadiliwe zaidi kabla halijafikishwa rasmi

(4) Kwa kuwa hakuwezi kuwa na amani ya kweli bila ya haki, na kwa kuwa amani ya Tanzania inashikiliwa na Waislamu walioruhusu dhulma hiyo, Waislamu tunayo dhima kubwa kwa kustawi kwa Mfumo Kristo ambao sasa hapana shaka yoyote unalisambaratisha Taifa. Lakini kama alivyosema Nyerere, anayedhulumiwa ni mtu anayeteseka. Asipopambana na huyo dhalimu, yeye ataendelea kuteseka wakati dhalimu anastarehe kwa amani. Akiamua kupambana, wote yeye na dhalimu watateseka.  


Baada ya miaka 50 ya kuachia kundi moja la jamii likistarehe na hali Waislamu wanateseka, umefika wakati sasa wa kugawana machungu ya udini tuliyoyabeba peke yetu kwa miaka hamsini.

NYERERE na SERIKALI 2: Natofautiana Naye katika Hili!

Nyerere: Hakika Namheshim Sana
 Nimesoma sehemu hii hapa Chini ya hotuba ya Nyerere kuhusu kuanzishwa kwa Serikali Mbili katika Jamuhuru ya Muungano wa Tanzania. Inawezekana ni kweli kwamba maelezo aliyokuwa anayatoa ya ukweli ndani yake, lakini ni ukweli pia kwamba yana Ombwe kubwa sana linaloacha maswali mengi ya msingi bila kujibiwa. 

Kwa Ufupi, namaanisha maelezo ya Nyerere kuhusu suala la Serikali Mbili - Ni Majibu Mepesi kwa Maswali Mazito! Inawezekana Nyerere hakuwa na majibu mazuri zaidi ya haya kwa wakati huo, au pia inawezekana kwa sababu alikuwa amezungukwa na watu ambao - aidha hawakuwa na UWEZO wa kuhoji au kurekebisha maamuzi yake binafsi - au HAWAKUWA NA UHURU wa kufanya hivyo. Hivyo matokeo yake ikawa kwamba kila atakalolisema yeye linafutiwa na makof mengi na vigeregere huku mkutano mzima ukiitikia kwa Sauti - ZIDUMU FIKRA ZA MWENYEKITI!

Maswala yangu ya Msingi

Kwanza: Nani aliamua Kuziunganisha Nchi hizi Mbili Zilizo Huru? 

Nyerere na Karume Wakisaini Hati ya Muungano
Kwa maelezo ya Nyerere, Tanganyika na Zanzibar "ZILIAMUA" kuungana! Sijui Nyerere aliposema "ziliamua" alikuwa anamaanisha nini? Kwamba ni Watu wa Wenye Nchi (wananchi) hizi mbili ndio waliamua au Ni VIONGOZI wa Nchi hizi Ndio waliamua?

Kama ni Viongozi Ndio waliamua - Basi Huu ulikuwa MSINGI MBOVU SANA wa kujengea Muunganoa wa Mataifa mawili YALIYO HURU! Muungano wa Nchi ni suala pana sana ambalo haliwezi kuachwa na kufanywa na Viongozi wachache wa KISIASA ambao wanatekeleza Ilani za Vyama vya Kisiasa - katika mataifa ambayo SI KILA RAIA ni mwanachama au hata kama ni "Mwanachama wa Kulazimishwa" - Basi SI Muumini wa vyama hivyo! 

Ndio maana LEO, ni muhimu sana suala la Muungano likarudishwa kwa wananchi wao ndio walijadili na kulitolea uamuzi. Kama Serikali ina wasiwasi kwamba wananchi hawatafanya maamuzi ambayo yenyewe inayaona ndiyoo "sahihi" basi ianze kwanza kwa kutoa elimu kwa wananchi kuhusu maamuzi gani yanaweza kuwa ni sahihi, lakini mwisho wa siku wnanchi ndio waamue wenyewe kipi ni sahihi!

PILI: Kumezwa kwa Zanzibar!

Karume
Nadhani kati ya hoja nyepesi MNO zilizo katika maelezo ya Nyerere ni suala la "Kumezwa" kwa Zanzibar kwa kisingizio cha Uchache wa Watu! Kwa kawaida, Nchi huendeshwa na MIFUMO, Mifumo ambayo kwa kawaida hutengenezwa kulingana na mahitaji ya Jamii/Taifa husika. Ni hoja nyepesi mno kusema ETI Zanzibar inaweza kumezwa kwa sababu ya Uchache wa Watu!

Nini kingefanyika?
Jambo lililotakiwa ilikuwa ni kuwekwa kwa mifumo mizuri ambayo ingehakikisha uwakilishi mzuri wa pande zote mbili katika ufanyaji wa maamuzi na katika uchangiaji wa gharama za huo Muungano! Taifa likiingia kwenye mahusiano au muungano na taifa lingine haliwezi kumezwa kutokana na Idai ya watu wake - litamezwa na mifumo isiyo mizuri ambayo hailipi nafasi ya kuonekana na kusikika katika hayo mahusiano!

TATU: Gharama za Kuendesha Muungano

Jambo la tatu ambalo halikuwa la Msingi kuliweka kama sababu ya Kuvunja Serikali ya Tanganyika na kuunda ya Muungano tu, lilikuwa ni suala la gharama. Kwa wakati huo (baada ya kuanzishwa kwa Muungano), hoja hii ilionesha mapungufu makubwa wakati wa uanzishaji wa muungano wenyewe. Kauli hii inamaanisha Mambo haya hayakufikiriwa wala kuzingatiwa kabla ya kuanzishwa kwa Muungano:


  1. Faida za Muungano: Katika hali ya kawaida, mtu hauwezi kuingia katika mahusiano pasipo kufanya mahesabu ya faida utakayoipata katika mahusiano hayo na iwapo faida hiyo inatosha kugharimikia Uendeshaji wa  Mahusiano hayo!
  2. Gharama za Kuendesha Mifumo itakayoundwa Chini ya Muungano: Suala la Nyerer kusema kwamba kuendesha Serikali ya Tanganyika ingekuwa gharama kubwa linaonesha ni kwa kiasi gani taathimini haikufanyika KABLA YA KUUNGANISHA NCHI kuona ni kwa kiasi gani Mifumo itakayozaliwa na Muungano (ikiwa ni pamoja na Serikali ya Muungano) itaweza kugharimikiwa. Hatua ya kuiua Serikali ya Tanganyika na kulivunja Bunge lake ilikuja kama Zimamoto ambayo ilitokana na kutokufanyika kwa taathimini ya kutosha kuuhusu Muungano husika kabla haujaundwa!
  3. Maelezo ya Nyerere yanaonesha kwamba haukufanyika Uchunguzi wa kina gharama za uendeshaji wa mifumo itakayoundwa chini ya Muungano - Huu ni upungufu mkubwa mno ambao unaleta matatizo hadi sasa kuhusu gharama za kuendesha muungano na Nani anufaike vipi na mapato yatokanayo na Muungano!
NNE: Hofu

Tayari Zanzibar Kuna Vurugu za Kuupinga Muungano!
Labla katika hoja zote zilizotumika kufanya maamuzi kuhusu nini kifanyike katika muungano, hakuna hoja isiyofaa kama ya "Hofu". Nyerere alisema ETI maamuzi ya kutengenza muundo uliopo wa Muungano YALITOKANA NA HOFU ya kumezwa kwa Zanzibar! Kama kuna jambo baya ambayo mtu anaweza akalifanya maisha yake basi ni kufanya maamuzi kutokana na hofu inayokuzunguka!

Kwa mara nyingine tena, HOFU hii ilitokana kwa kiasi kikubwa sana na Kutokuwashirikisha Wananchi katika Kufanya maamuzi - hivyo walioyafanya WALIOGOPA iwapo maamuzi yatakuwa mzigo wa gharama kwa wananchi - wananchi wanaweza kuinuka na kuyapinga! 

Na kwa upande mwingine, Hofu hii ilitokana na kutokufanyika kwa taathimini ya kina kuhusu gharama, faida na mahitaji mengine ya kuuendesha Muungano. Taathimini hiyo ingefanyika mapema, hakika tusingehitaji kufanya maamuzi kwa "Hofu" ya kitu Chochote!

Kweda Mbele....

Kimsingi, binafsi napenda uwepo wa Muungano, na ningependa uendelee. Tatizo kubwa lilipo ni kwamba Muungano wetu huu wa sasa Umejengwa kwenye MSINGI MBOVU ambao hauwezi kuuhakikishia huu Muungano UENDELEVU wake!

Najua kubomoa ni rahisi kuliko Kujenga, ndio maana wengi hupenda kukimbilia wazo la kuuvunja Muungano kuliko kutumia akili na nguvu zao kufikiria namna ya kuuboresha! 

Maoni ya Wananchi zamu hii LAZIMA yatumike Kuamua Hatma ya Muungano
Binafsi nalishauri taifa - kwa uongozi wa Serikali kubadilisha mawazo yake ya Sasa ya Hofu na Wasiwasi kuhusu maamuzi ya Wananchi. Serikaoli yetu - Iwapo inao uwezo wa kufanya hivyo - Inatakiwa ijipange zivuri na kuliwasilisha hili suala RASMI kwa wananchi kwa ajili ya kulijadilia na kulifanyia maamuzi.

Kitendo cha Serikali kulikwepesha suala hili lisiwemo kwenye Mjadala wa Katiba Mpya haimaanishi kwamba ndo inajihakikishia kwamba Muungano utadumu. Hali ikiendelea hivi kuna siku wananchi watagoma kuendelea kufanya jambo lingine lolote mpaka Suala la Muungano likizungumzwa na kufanyiwa maamuzi. Ikifikia huko, Ni hakika Nafasi hata ile ndogo iliyopo sasa ya Kuulinda na kuudumisha Muungano itakuwa imeshapotea, na HAKIKA, MUUNGANO UTAVUNJWA!




HOTUBA YA NYERERE AKIFAFANUA KUUNDWA SERIKALI 2 NA SIO 3 TANZANIA


Nchi mbili zinapoungana na kuwa nchi moja mifumo ya kawaida ya katiba ni miwili;

Muungano wa serikali moja, au shirikisho la serikali tatu. Kwa mfumo wa kwanza kila nchi itafuta serikali yake,na nchi mpya inayozaliwa itakuwa ni nchi moja yenye serikali moja. Katika mfumo wa pili kila nchi itajivua madaraka Fulani ambayo yatashikwa na serikali ya shirikisho na itakuwa na serikali ambayo itakuwa na mamlaka juu ya mambo yaliyobaki.

Mambo yatakayoshikwa na serikali ya shirikisho ni yale ambayo yakibaki katika mamlaka ya nchi zilizoungana, basi kwa kweli nchi hizo zitakuwa hazikuungana kuwa nchi moja, basi zinaendelea kuwa nchi mbili zenye ushirikiano mkubwa katika mambo Fulani Fulani. Nchi za Afrika Mashariki zilikuwa katika hali kama hiyo kabla ya kuvunjika kwa jumuiya ya Afrika ya Mashariki. Zilikuwa ni nchi tatu zenye ushirikiano mkubwa, lakini hazikuwa nchi tatu zilizoungana kuwa Nchi moja yenye muundo wa shirikisho. Shirikisho halisi la nchi mbili litakuwa ni nchi moja yenye serikali tatu, serikali ya shirikisho, na serikali mbili za zile nchi mbili za awali zilizoungana kuzaa nchi mpya moja.

Tanganyika na zanzibar zilipoamua kuungana na kuwa Nchi moja, tungeweza kufuata mmojawapo wa mifumo hiyo ya kawaida. Lakini tulishindwa kufanya hivyo kwa sababu ya udogo wa Zanzibar na ukubwa wa Tanganyika. Zanzibar ilikuwa ina watu laki tatu (300,000) na Tanganyika watu milioni kumi na mbili (12,000,000).

Muungano wa serikali moja ungefanya ionekane kama Tanganyika imeimeza Zanzibar. Tulikuwa tunapigania Uhuru na Umoja wa Afrika; hatukutaka tudhaniwe, hata kwa makosa, kwamba tunaanzisha ubeberu mpya! Kwa hiyo mimi nilipinga mfumo wa serikali Moja na Shirikisho la serikali tatu lingekuwa ni gharama kubwa mno kwa Tanganyika. Zanzibar ingeendesha  serikali yake na kuchangia gharama za kuendesha serikali ya shirikisho; na Tanganyika ingefanya vivyo hivyo. Lakini ni dhahiri kwamba mchango wa Tanganyika ndio hasa ungeendesha serikali ya shirikisho.

 Kwa hiyo Tanganyika ingeendesha serikali yake ya watu 12,000,000 na pia ndiyo ingetoa sehemu kubwa ya kuendesha serikali ya shirikisho la watu 12,300,000. Ni watu wanaofikiri kwa ndimi zao wanaodhani kuwa gharama ya serikali yoyote kati ya hizo ingekuwa ndogo. Gharama ya serikali ya Tanganyika isingekuwa ndogo, (waulizeni wazanzibari) na wala ya serikali ya shirikisho isingekuwa ndogo, hata bila gharama za mambo yasiyo ya shirikisho. Na gharama zote hizo kwa kweli zingebebwa na Tanganyika.

Kwa hiyo ilitupasa tujiulize kwa nini tunataka kuibebesha Tanganyika gharama zote hizo; na hasa kwa nini tunataka Serikali  ya Tanganyika? Hivi tuna hofu ya kwamba Tanganyika, bila kuwa na serikali yake, itaonekana kuwa imemezwa na Zanzibar? Hofu yetu ni kwamba tukiwa na serikali moja Tanganyika itaonekana kuwa imeimeza Zanzibar. Basi na tutafute muundo ambao utaiondolea Zanzibar hofu hii ya kumezwa, bila kuibebesha Tanganyika mzigo wa kuendesha serikali mbili zenye uzito unaolingana.

Hivyo ndivyo tulivyofanya, na hiyo ndiyo asili ya muundo wa muungano wa serikali mbili. Badala ya kutungua mfumo uliopo kama wapumbavu, tulitazama hali halisi yetu ilivyokuwa, na tukabuni mfumo utakaotufaa zaidi.

IDD SIMBA Aburutwa Mahakamani!

Idd Simba















 
Tausi Ally na James Magai MWENYEKITI wa Bodi ya Shirika la Usafiri  Dar es Salaam (Uda) Ltd, Iddi Simba, jana alipandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu akikabiliwa na mashtaka manane, likiwemo la matumizi mabaya ya madaraka na kulisababishia shirika hilo hasara ya Sh2.4 bilioni.Mbali na Simba ambaye aliwahi kuwa Waziri wa Viwanda na Biashara, washtakiwa wengine ni Meneja Mkuu wa Uda, Victor Milanzi na Mkurugenzi wake Salim Mwaking’inda ambaye pia aliwahi kuwa Diwani wa Kata ya Sinza (CCM).

Baada ya Mwendesha Mashtaka wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Benny Lincoln kumaliza kuwasomea mashtaka yanayowakabili, aliieleza mahakama hiyo kuwa upelelezi wa kesi hiyo umeshakamilika na wanaomba kesi ipangiwe tarehe ya kutajwa kabla ya kupangiwa  tarehe ya maelezo ya awali. Wakili Said El- Maamry anayemtetea Simba na mwenzake, Alex Mgongolwa waliiomba Mahakama impatie dhamana mteja wao hoja ambayo haikuwa na pingamizi kutoka kwa Lincoln ambaye alisema mashtaka yanayowakabili washtakiwa yanadhaminika.

Ili kujidhamini, Hakimu Mfawidhi, Ilvin Mgeta aliwataka washtakiwa kutoa hati ya nyumba na kuwa na wadhamini wawili wanaoaminika, kila mmoja wao asaini bondi ya Sh500 milioni.

Baada ya kutolewa kwa masharti hayo, Simba aliwasilisha hati ya nyumba yenye thamani ya Sh8 bilioni na kuridhia wenzake waitumie kupata dhamana.

Uchunguzi wa gazeti hili umebaini kuwa hati hiyo ya nyumba ni ya kiwanda cha Kays Hygiene Products Ltd, kilichoko Mikocheni eneo la Viwanda, Plot namba 23, kinachomilikiwa na Simba na mkewe Khadija.

Simba ni Mwenyekiti wa Taasisi ya mikopo kwa Wajasiriamali ya Pride (T) Ltd na Mwenyekiti wa Wazee wa Mkoa wa Dar es Salaam. Akisoma hati ya mashtaka jana Lincoln alidai kuwa  Septemba 2, 2009 Dar es Salaam, Simba na Milanzi  walikula njama ya kuchepusha fedha kinyume na Kifungu cha 29 cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Sura ya 11 ya 2007.

Lincoln alidai kuwa Simba na Milanzi walighushi barua  wakionyesha kuwapo kwa kiwango zaidi cha fedha kwenye akaunti zote za benki za Uda wakati wakijua kuwa si kweli. Aliongeza kuwa siku hiyo hiyo, Simba na Milanzi kwa pamoja, walichepusha Sh320 milioni wakijifanya ni malipo ya awali ya mauzo ya hisa katika shirika hilo fedha ambazo walijipatia kutokana na nyadhifa zao.

Aidha, kati ya Septemba 3, 2009 na Machi 31, 2010, Simba na Milanzi wanadaiwa kujipatia Sh320 milioni kwa njia ya udanganyifu kutoka kwa Robert Simon Kisena wakijifanya ni sehemu ya malipo ya hisa za Uda. Lincoln alidai kuwa washtakiwa Simba na Mwaking’inda kati ya Septemba 2009 na Februari 2011, wakati wakitekeleza majukumu yao, kwa makusudi walitumia vibaya nafasi zao waliharibu hisa  milioni 7,880,330 zisizotumika za Uda ambalo ni shirika linalomilikiwa kati ya Serikali Kuu na Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam zinazokadiriwa  kuwa na thamani ya Sh1,142,643,935  bila kufuata taratibu za zabuni kitendo ambacho ni uvunjwaji wa masharti ya Kanuni ya 63 (1) ya Ununuzi ya umma.

Washtakiwa hao wote kwa pamoja wanadaiwa kuwa  kati ya Septemba 9 na Februari 11, 2011 wakitekeleza majukumu yao, kwa makusudi walitumia vibaya madaraka yao kwa kugawanya hisa 7,880,330  zisizotumika za UDA kitendo ambacho ni uvunjwaji wa masharti ya vifungu vya ushirikiano katika kampuni  na Kifungu cha 74 cha Sheria ya Makampuni Sura ya 212 iliyorekebishwa mwaka 2002.

Mwendesha mashtaka huyo wa Takukuru, alidai kuwa Februari 11, 2011 washtakiwa hao walishindwa kuchukua tahadhari zinazostahili, walimuuzia Simon hisa milioni 7,880,303 zisizotumika za Uda kwa bei ya Sh1,142,643,935  bila kufuata utaratibu wa zabuni ambao ungeweza kutoa nafasi kwa mnunuzi kutoa ofa ya bei inayolingana na thamani ya hisa hizo, jambo ambalo liliisababishia Uda hasara ya Sh2,378,858,878.80.