Tuesday, May 22, 2012

JIFUNZE SIASA: Siasa ni Zaidi ya Ushabiki wa Vyama!


Katika hatua nyingine, tafakari ya leo inalenga kutoa elimu zaidi ya Siasa kwa wadau siasa.

Kutokana na sababu mbalimbali za kisiasa, siasa za Tanzania kwa sasa zimejikita zaidi katika vyama vya siasa na makundi ya kisiasa ndani ya vyama hivyo. Pamoja na kwamba sababu mojawapo kubwa ni kutokuruhusiwa kwa watu kufanya kkugombea nafasi za kisiasa binafsi (pasipo kuhitaji kupitia kwenye vyama), lakini pia uelewa wa wananchi kuhusu siasa umechangia katika kuifanya hali kuwa hivi ilivyo.

Katika siasa za Tanzania kwa sasa, kila mtu akiongelea au kujadili suala fulani la kisiasa, watu hutaka kwanza kuelewa yeye ni wa"Chama gani" au anatetea Chama gani au Anapinga chama gani. Watu wengi Tanzania wanaoshiriki kwa namna mbalimbali katika siasa hawajui kwamba Siasa ni pana zaidi ya Vyama vya siasa. Kuna mambo kadhaa ya muhimu kuyaelewa hapa:

Kwanza: Siasa kama Taaluma

Kuna watu wengi ambao hawaelewi kuwa Siasa ni taaluma ambayo husomewa na kufundishwa katika Shule na Vyuo mbalimbali - hadi vyuo vikuu. Kwa sababu hiyo, kuna watu wanaofanya Siasa kama Wanazuoni, Wasomi, Wataalam, Watoa Elimu na Wachambuzi wa Siasa. Watu hawa sio lazima wawe katika vyama vya siasa ili waweze kujadili, kujadili, kuelimisha au kukosoa masuala ya kisiasa.

Pili: Siasa katika Vyombo vya Habari

Ni muhimu pia kuelewa kwamba mtu anaweza kushiriki katika Siasa kama mwanahabari na mchambuzi wa habari katika vyombo vya habari. Mtu huyu pia - japo anaweza kuwa na chama chake cha siasa - lakini SIO lazima awe mwanachama wa chama fulani cha Siasa.

Ni muhimu pia kuelewa watu hawa wote - katika kundi la kwanza na la pili wanaweza wakasifu au wakapinga au hata kukemea baadhi ya mambo yanayofanywa na vyama vya siasa. Mtu anapokisifia chama kimoja cha Siasa - SIO LAZIMA kwamba awe mwanachama wa Chama hicho au anakipinga kingine!

Tatu: Siasa katika Vyama vya Siasa

Kundi hili la watu wanaofanya Siasa kupitia vyama vya siasa ndilo maarufu zaidi hapa Tanzania. Hii ni kwa sababu - kama ilivyoelezewa hapo juu - na Sheria za Uchaguzi ambazo hairuhusu wana siasa kugombea nafasi za kisiasa pasipo kupitia katika vyama vya siasa.

Nne: Wanasiasa Binafsi

Hili ni kundi la watu ambao huweza kufanya siasa, na hata kugombea na kupata nafasi za kisiasa kama Udiwani, Ubunge au hata Urais pasipokuwa mwanachama wa chama chochote cha siasa.

Katika nchi ambazo sheria zake zinaruhusu kuwa na wagombea binafsi, watu huwa na sera na milengo yao ya kisiasa ambayo huielezea kwa umma wakati wa kampeni na huweza kupigiwa kura na kuchaguliwa katika chaguzi mbalimbali kwa kuzingatia sera zao na uwezo wao binafsi kuongoza na kutekeleza majukumu yao ya kisheria na kikatiba pasipokuhitajika kuwa chini ya chama fulani cha kisiasa.

Hali Ilivyo Tanzania

Kutokana na Sheria za Uchaguzi Tanzania kutoruhusu kuwepo kwa wagombea binafsi, hali hiyo imeathiri kwa kiasi kikubwa sana hata namna watu wanavyoielewa na kuichukulia siasa. Mazoea hayo ambayo yametokana na sheria kandamini inayowanyima wananchi haki yao ya kikatiba ya kutokulazimishwa kujiunga katika vyama - imewafanya Watanzania kuelewa na au kudhani kwamba kila mtu anayezungumzia masuala ya siasa au kuyatolea mawazo, tafakari au mtazamo basi NI LAZIMA awe mwananchama wa chama fulani cha siasa - SIO SAHIHI!

Nchini Tanzania leo mtu akitolea maoni jambo fulani la Kisiasa - Iwe kwa mazungumzo au maandishi - jambo la kwanza Mashabikiwa vyama wanalotaka kuliona ni kuelewa yeye yuko Chama gani? Kwa bahati mbaya sana, uelewa huu wa chama cha mtu watu huwa wanautumia vibaya.

Katika Siasa za Tanzania ambazo kwa sasa zimejaa ushabiki, watu hutumia vibaya utambulisho wa vyama wanapoupata. Katika ushabiki wa siasa za Tanzania, watu wakishajua Chama cha Mtu, huwa wako tayari kumtetea na kulinda kila atakalolisema au kulitolea maoni - hat akama kimsingi halifai!

Na kwa Upande wa pili ni hivyo hivyo - watu wakishajua msemaji sio wa Chama chao, wako tayari kupinga na kukataa kila atakalolisemea au kulitolea maoni - hata liko sahihi na lina manufaa. HIZI SIO SIASA SAHIHI KWA MAENDELEO YA TAIFA!

Watu katika Tanzania ya Leo wameweka na wanazidi kuweka vyama vyao vya siasa kuliko ukweli na usahihi wa masuala ya kitaifa yanayojitokeza katika siasa. HII SIO SAHIHI! Kila ukitoa tamko au mtazamo kuhusiana na suala fulani la kisiasa - watu watalazimishia mpaka waliunganishe na Chama fulani! Hii sio Siasa!

Tuende wapi Tanzania

Njia sahihi tunayopaswa kuichukua Watanzania inahusisha masuala kadhaa - muhimu ikiwa ni haya yafuatayo:

Siasa Kwa Maendeleo: Tuhakikishe Masuala yote ya Kisiasa tutakayoyasimamia, kuyatetea na kuyasifia yawe yanawasimamia na kuwakilisha Maslahi ya Taifa na Watanzania wote kwa ujumla - bila kujali Chama au kikundi fulani cha Siasa! Tukubali Hoja, Mitazamo  na Sera zile tu ambazo mwishoni zitazaa matunda kwa Taifa zima na kwa Watanzania wote!

Siasa za Umoja: Tusimamie siasa ambazo zitajenga ummoja wa kitaifa na kuweka maslahi yetu sote kwa pamoja mbele. Tukatae siasa zitakazolenga kututenga na kutugawa kwa makundi, makabila, dini au vyama. Tuhakikishe tunashika na kufanya siasa ambazo pamoja na tofauti za kisera, hoja na mawazo - bado zitaendelea kutuunganisha sote kama Watanzania katika masuala ya msingi ya kitaifa.

Siasa za Ukweli: Tukatae uongo katika siasa zetu. Tuutafute na kuusimamia Ukweli katika siasa zetu. Tuukatae Uongo - hata kama utatoka katika vyama na makundi yetu! SIASA SIO UONGO, japo inaweza kutumiwa na WAONGO na wakajaribu kuhalalisha Uongo wao kama jambo halali kisiasa! TUKATAE SIASA HIZO! Siasa zetu - iwe ni watu binafsi, Vyama au Makundi - Zisimamie ukweli wa yale tunayoyasema na yale tunayoyafanya. TUUKATAE UONGO HATA KAMA UTASEMWA AU KUFANYWA NA WATU WA VYAMA VYETU AU MAKUNDI YETU!

Tanzania inaweza ikapata maendeleo makubwa ya Kiuchumi na Kijamii kama zilizvyo nchi nyingine tajiri duniani, lakini hilo halitawezekana iwapo hatutajenga msingi imara na bora wa Siasa zetu! Tunahitaji kuhakikisha kuwa sote kwa pamoja na tunaelewa ni aina gani ya Siasa ambazo zinaweza kulisaidia taifa letu kuendelea na kuzifuata hizo.

TANZANIA INANITEGEMEA MIMI NA WEWE - Timiza Wajibu Wako!

7 comments:

  1. funguajicho.blogspot.comMay 22, 2012 at 11:51 PM

    Nakubaliana na wewe juu ya siasa. Ni kweli tunahitaji siasa za maendeleo na wala si maslahi ya makundi au watu fulani. Bahati mbaya sana, wanasiasa wetu ni wachache sana ambao wanawaza kama wewe unavyosisitiza. Nataka niseme, kwa maoni yangu, JANUARI MAKAMBA, ZITTO KABWE, DR. SLAA, MAGUFULI, ni kati ya wanasiasa wachache sana ambao huoni ukakasi wa uchama katika matendo na maneno yao. Lakini mitizamo yao kwa kiasi kikubwa inachukiwa sana na wanaotutawala. Sijui ni lini tutakomaa, ila bado tuna safari ndefu.

    ReplyDelete
  2. Funguajicho, asante kwa maoni yako... Wakati wa Kukomaa unaanza sasa, tuanze kwa kuwaunga mkono wale tunaoona wanasimamia maslahi ya Taifa zaidi, na tuzidi kuwatenga wanaotanguliza matumbo yao na vyama vyao, kuna siku watakuja kujibaini wamebaki peke yao - na watatufuata katika Ujenzi wa taifa!

    ReplyDelete
  3. Umesomeka Mussa nami nakuunga mkono sana kwa somo hili. Ni wakati ,muafaka wa kuwaunga mkono wale ambao wanasimamia maslahi ya taifa kuliko kusimamia maslahi ya chama na wao binafsi. Tukisha kuwaunga mkono nina uhakika mtazamo wa hao wachache hautakuwa na nafasi katika jamii yetu.

    ReplyDelete
  4. Umesomeka Mussa nami nakuunga mkono sana kwa somo hili. Ni wakati ,muafaka wa kuwaunga mkono wale ambao wanasimamia maslahi ya taifa kuliko kusimamia maslahi ya chama na wao binafsi. Tukisha kuwaunga mkono nina uhakika mtazamo wa hao wachache hautakuwa na nafasi katika jamii yetu.

    ReplyDelete
  5. safi sana Mussa kwa makala hii yenye mafunzo ,wengi wa watanzania tumechukulia siasa kwa ushabiki wa vyama tu kiasai kwamba hata kama chama kitakosea au mwanachama akikosea basi watu hawaporadhi kukemea badala yake ni ushabiki tu .LAZIMA TUBADILIKE.

    ReplyDelete