Thursday, May 31, 2012

"NAPE Ni GAMBA Linalotakiwa Kuvuliwa!" - MAIGE


Akizindua matawi mawili ya wakereketwa wajasiriamali wa CCM katika Kijiji cha Isaka, Kahama, Shinyanga, Maige ambaye ni Mbunge wa Msalala alimtaka Nape kuacha tabia yake ya kutoa kauli ambazo kwa namna moja au nyingine zinaelekea kukidhoofisha chama.

Alimtaka kupima utendaji wake tangu alipoishika nafasi hiyo ya Itikadi na Uenezi na kujiuliza ni wanachama wangapi wameingia ndani ya chama hicho.

Alisema sasa hivi kuna wimbi kubwa la wanachama wa chama hicho kuhama na kukimbilia upinzani na kusema ni wajibu wa Nape kupima na kuona kuwa kazi ya itikadi na uenezi haiwezi na kwani hajui wajibu wake akisema ni mtu wa kumhurumia.

Maige alisema mbali ya kushindwa kuzuia wimbi la wanachama kukihama CCM pia hapaswi kuvumiliwa kutokana na kauli yake kwamba hata kama wanachama watahama wote na akabaki yeye (Nape) peke yake, haitakufa. Alisema kauli hiyo haikijengi chama, bali kuchochea makundi ambayo yanaweza kukibomoa.

Alisema akiwa mwana CCM anaona kwamba sasa hivi Nape amekuwa hafanyi kazi ya uenezi na kukirejeshea haiba na mvuto ambao umepotea kwa wananchi na kwamba, kazi anayoifanya sasa ni kukuza makundi na kusema ovyo.

Aliendelea kumshambulia Nape kwa maneno akisema amejenga jeuri, kiburi, dharau na ulevi wa madaraka huku akidai kwamba kitendo cha CCM kupoteza wanachama zaidi ya 10,000 kwa wakati mmoja mkoani Arusha na sehemu nyingine wanachama 3,000 ni ishara ya hatari lakini, Nape amekuwa akiwaita wanaohama kwamba ni mzigo.

“Huyu Nape ni lazima atupishe. amekifanya chama kama mali yake, yeye ndiye mwenye jukumu la kueneza sera za chama na kutafuta wanachama wapya, lakini ndiyo kwanza anasema waachwe waondoke, Chadema wanatamba kila siku yeye hajali, huyu nasema ni gamba ni bora atupishe,” alisema.

Baada ya mashambulizi hayo, Maige alijitetea kwamba maneno yake dhidi ya Nape yasitafsiriwe kama ni kuulilia uwaziri: “Ni uchungu nilionao kwa chama changu kuona kila siku zinavyokwenda ndivyo tunavyopoteza idadi kubwa ya wanachama, tuliyemkabidhi jukumu la uenezi anasema hajali, sasa huyu si atupishe mapema kabla mambo hayajaharibika?”

“Nikuombe Mwenyekiti wa CCM Mkoa mzee wangu, Mgeja (Hamis), nafikiri ninyi wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (Nec ya CCM) mnapaswa kuchukua hatua haraka juu ya Nape... huyu sasa ni tatizo. Chama kitawafia hivihivi mkiona, avuliwe gamba maana tukisubiri ajivue atatuchelewesha, CCM ni wanachama si Nape.”

Wakati Maige akitoa maneno hayo, Mgeja alikuwa ameinamisha kichwa chake chini huku mikono ikiwa kichwani, lakini wana CCM na wananchi wengine walikuwa wakishangilia.

Aidha, Maige aliwalaumu viongozi wa CCM katika ngazi ya wilaya na kata ambao wamekuwa na tabia ya kutowatembelea wananchi katika maeneo yao kusikiliza kero zao wakisubiri mpaka viongozi wa kitaifa ndipo na wao wajitokeze.

“Jamani inakuwaje kiongozi mwenezi wa CCM kata ama wilaya anakaa kimya kabisa hakuna kazi yoyote anayoifanya! Viongozi wa aina hii wasipewe nafasi kabisa katika uchaguzi ujao. Tupate safu ya viongozi wenye kukifia chama chetu.”

“Maana kama watu wanakuja na Operesheni Sangara hakuna anayesimama kujibu, Operesheni Vua Gamba Vaa Gwanda hakuna aliyewajibu wala CCM haijatafuta operesheni yoyote ile kukabiliana nao, sasa wameanza Operesheni Movement For Change (M4C), sisi na Nape wetu kimya tunawaangalia tu wanazoa wanachama. Tuwe makini chagueni viongozi wenye uchungu na chama,” alisema Maige.

Alipotakiwa kuzungumzia tuhuma hizo za Maige, Nape alisema: “Nasubiri taarifa rasmi ya chama na nikiyakuta hayo nitajibu. CCM ina taratibu zake katika utendaji wake wa kazi. Katika taratibu hizo, ziara zote za viongozi wetu zinaandikiwa taarifa ambayo lazima zipite kwangu. Hayo unayosema yakinifikia, nitayajibu lakini siwezi kuzungumza bila hakika kwamba amesema.”

Bonyeza Hapa Ilikusoma Makala Inayozungumzia Utendaji wa Nape katika Nafasi aliyonayo Na Jinsi ambavyo unaweza kukiponza Chama cha Mapinduzi

Taarifa hii ni sehemu ya Taarifa ya Gazeti la Mwananchi, May 31 2012!

No comments:

Post a Comment